Maisha ni mchakato mrefu na uliojificha wa mafanikio kufikia kusudi letu hapa duniani. Kuna majira maisha yanaonekana wazi kujaribu zaidi ya nguvu zetu. Hujaribu uvumilivu wetu, imani yetu, nidhamu yetu, na uelewa wetu wa mchakato huu.
Kipindi hiki huenda kikawa ni majira ya uchungu — nyakati ambapo juhudi hazionekani, sala huonekana kutojibiwa, na hata maendeleo yetu hayaonekani. Ni majira ambapo kiongozi hubeba jukumu kubwa bila shukrani.
Ni kipindi ambacho mwenye ndoto anajaribu kufikia malengo yake licha ya kukatishwa tamaa mara kwa mara. Anamka kila siku akiwa ameazimia kusonga mbele huku akipambana na uchovu, kutokuwa na uhakika, na shinikizo kubwa ndani yake.
Kwa ulimwengu wa nje, anaweza kuonekana kama hakuna anachopitia. Lakini ndani ya nafsi yake anapitia changamoto kubwa.
Ukweli mmoja mkubwa kuhusu maisha ni huu: si kila kitu muhimu hutokea kwa mara moja. Dunia inaelewa kanuni hii. Mbegu haiwi mmea mara moja. Hutoweka kwanza gizani, ikizikwa chini ya ardhi ambapo hakuna mtu anayeona wala kupongeza ukuaji wake. Lakini katika mahali hapo pa siri, mizizi huota, nguvu hukua, na maisha huanza kimya kimya hadi siku ambayo itachipuka juu ya ardhi.
Vile vile huu ndiyo ukweli kwa maendeleo ya binadamu, uongozi, na hatima yake. Baadhi ya mabadiliko muhimu zaidi maishani hutokea kimya kimya. Hekima hukua kimya. Nidhamu hujengwa kimya kimya. Uponyaji hutokea kimya kimya. Ukomavu hukua kimya kimya. Hata Mungu mara nyingi hufanya kazi zake kimya kimya.
Janga la jamii ya sasa ni kwamba watu wengi wamekuwa waraibu wa kuonekana. Tunaishi katika ulimwengu unaoshangilia kelele, kasi, na mafanikio ya haraka ya papo hapo.
Watu wanataka mafanikio yanayoonekana bila kuelewa maandalizi yasiyoonekana ya mafanikio hayo. Wanavutiwa na matokeo huku wakipuuza mchakato. Wanasherehekea mavuno huku wakisahau majira ya kupanda, kusubiri, na uvumilivu yaliyowezesha mavuno hayo.
Lakini cha kushangaza, maisha hayatoi subira na muda wa kutosha. Mafanikio yetu mengi hujengwa kupitia njia za mkato na kelele. Lakini mafanikio ya kweli hujengwa polepole, kimya kimya, na mara nyingi kwa uchungu. Uongozi bora na imara ni kielelezo cha ukweli huu haswa.
Nyuma ya kila taasisi imara kuna kiongozi aliyevumilia usiku bila kulala, maamuzi magumu, kukatishwa tamaa, kukosolewa, na shinikizo la kimya kimya. Nyuma ya kila maono yanayoheshimiwa kuna mtu ambaye aliendelea kuamini muda mrefu kabla ya wengine kuona kinachowezekana. Nyuma ya kila urithi wenye maana kuna sadaka ambayo umma huenda usiielewe kikamilifu.
Watu wengi wanavutiwa na uongozi kwa sababu wanaona ushawishi. Wachache wanaelewa mzigo wa kihisia unaokuja na uwajibikaji.
Kiongozi anaweza kutumia miaka mingi akiwajenga watu na bado akapitia usaliti. Anaweza kujitolea ili kutoa fursa kwa wengine na bado akabaki kutokueleweka. Anaweza kubeba uzito wa taasisi huku akipambana na hofu, uchovu, na kutokuwa na uhakika.
Na bado, licha ya haya yote, kiongozi wa kweli anaendelea. Anaendelea kwa sababu uongozi haupimwi kwa maneno. Unapimwa kwa uwajibikaji. Uongozi halisi haupimwi wakati makofi yanapopigwa na kushangiliwa bali kwa mifumo inayofanya kazi vizuri. Uongozi imara hujaribiwa wakati wa ukimya - wakati maendeleo yanapatikana taratibu, wakati shinikizo linapoongezeka, wakati misaada ni hafifu na wakati jaribu la kukata tamaa linapokuwa na shinikizo. Ni wakati huo ambapo tabia hufunuliwa. Kwa sababu nyakati ngumu hufichua tofauti kati ya watu waliojitolea kweli na watu waliojitolea kwa ajili ya manufaa yao tu binafsi.
Kuna majira ambapo maisha ni magumu. Unafanya kazi kwa bidii lakini huoni mafanikio yoyote. Unasali kwa bidii lakini hupati majibu ya haraka. Unajenga kwa uvumilivu lakini matokeo yanabaki kuwa madogo. Katika nyakati kama hizi, unaweza kukata tamaa kimya kimya. Unaanza kuhoji umuhimu wako, kujitoa kwako, na hata thamani yako. Lakini labda kinachoonekana kama kuchelewa inaweza kuwa ni maandalizi. Labda maisha yanakuandaa kwa kitu kikubwa zaidi. Labda Mungu anakufundisha nidhamu kabla ya kupanua uwezo wako. Labda baadhi ya milango inabaki imefungwa kwa sababu bado unajiandaa kwa kile kilicho nyuma ya milango hiyo. Kwa maana mafanikio bila ukomavu na utayari yanaweza kumwangamiza mtu kwa haraka kuliko kushindwa au kukosa kungeweza.
Hii ndiyo maana majira ya kimya hayapaswi kamwe kudhaniwa ni majira matupu yasiyokuwa na faida. Ni majira ya ujenzi. Majira ambapo misingi imara inajengwa. Majira ambapo uvumilivu unakuzwa. Ambapo hekima huimarishwa. Ambapo uvumilivu hujaribiwa. Ambapo nguvu ya kihisia huundwa.
Mkulima anaelewa ukweli huu vizuri. Hachimbi mbegu alizopanda mwenyewe kila asubuhi ili kudhibitisha jinsi mbegu hiyo inavyoota. Anaamini katika mchakato. Anaelewa nyakati na majira. Anaelewa kwamba aina fulani za mazao huchukua muda mrefu kabla ya mavuno.
Hata hivyo, wanadamu walio wengi mara nyingi huenda kinyume na kanuni hii. Tunataka ushahidi wa haraka. Tunataka uthibitisho wa haraka kwamba kujitoa kwetu kuna faida.
Lakini maisha hutufundisha mara kwa mara kwamba vitu vyenye thamani zaidi huchukua muda kustawi. Mti unaokua haraka sana hukua na mizizi dhaifu. Kiongozi anayeinuka haraka sana mara nyingi hukosa hekima ya kuongoza. Mtu anayepata mafanikio bila misingi imara na nidhamu hatimaye huanguka juu ya uzito wa mafanikio yake mwenyewe. Hii ndiyo sababu misingi imara ni muhimu zaidi kuliko matokeo ya haraka. Na misingi imara kwa kawaida hujengwa kimya kimya.
Pia kuna somo la kiroho lililofichwa ndani ya ukweli huu. Mara nyingi, wakati wa misimu migumu zaidi ya maisha, watu hudhani Mungu hayupo kwa sababu mbingu inaonekana kimya. Lakini ukimya huu si kutokuwepo kwa Mungu.
Kutokuwepo kwa mwendelezo katika maisha yako haimaanishi kutokuwepo kwa kazi ya kimungu. Baadhi ya baraka zinaandaliwa zaidi ya uwezo wako. Baadhi ya vita vinapiganiwa kwa ajili yako bila wewe kujua. Baadhi ya matukio ya kukata tamaa kwa kweli inaweza kuwa ni ulinzi uliofichwa. Baadhi ya ucheleweshaji ni sababu za kimungu na si sababu ya kukataliwa.
Na wakati mwingine, unapojitahidi kuelewa mchakato huu, Mungu anaumba kimya kimya ndani yako mtu halisi unayehitajika kuwa kabla ya maisha yako mapya kuanza.
Siku moja, matokeo ya majira haya ya kimya yataonekana. Watu wanaweza kuiita bahati, neema, mafanikio ya usiku mmoja, au bahati mbaya. Wanaweza kuvutiwa na mafanikio yanayoonekana bila kuelewa mchakato usioonekana nyuma yake.
Lakini utakumbuka. Utakumbuka usiku wa upweke. Vita vya ndani. Sadaka ambazo hakuna mtu aliyeziona. Shinikizo ulilobeba kimya kimya. Nyakati ambazo karibu ulikata tamaa lakini hata hivyo ukachagua kuendelea. Na labda hapo ndipo shukrani za dhati inapoanzia — utambuzi kwamba hata wakati wa misimu yako isiyo na uhakika, Mungu bado alikuwa akifanya kazi kimya kimya kwa ajili yako.
Somo
Usipime maendeleo yako kwa matokeo yanayoonekana tu. Baadhi ya mabadiliko makubwa katika uongozi na maisha hutokea kimya kimya kabla hayajatokea hadharani. Majira ya ukimya si misimu isiyo na maana; ni majira ya maandalizi. Jifunze kuamini katika mchakato, kubaki na nidhamu wakati wa shida, na kuelewa kwamba misingi imara mara nyingi hujengwa mbali na makofi. Kwa maana katika uongozi, katika hatima, na katika maisha yenyewe, Mungu mara nyingi hufanya kazi Yake kubwa zaidi kimya kimya.
No comments:
Post a Comment